Kutoka kushoto: Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye akisikiliza hotuba wakati wa ibada ya kumkumbuka mpigania haki mashuhuri na Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela. Aliyeketi kulia kwake ni Mwanasiasa Mkongwe Kingunge Ngombale Mwiru, akifuatiwa na Balozi wa Algeria hapa nchini, Djelloul Tabet na mwakilishi wa watu wa Palestina, Nasir Abujaish.
Dar es Salaam. Wasomi na watu mbalimbali wamesema
katika kumwenzi Rais wa Kwanza Mzalendo wa Afrika Kusini, Hayati Nelson
Mandela ni kutekeleza yote aliyofanya kwa vitendo siyo kuomboleza kwa kulia.
Pia, walisema viongozi wa Bara la Afrika wanatakiwa kutambua
kuwa uongozi ni dhamana ya wananchi na hawana budi kuepuka kutumia madaraka
kujineemesha wao na familia zao.
Hayo yalisemwa jana wakati kumbukumbu ya Mandela, iliyoandaliwa
na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na kuhudhuriwa na watu mbalimbali wakiwamo
wasomi, wanasiasa na mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini.
Kada wa CCM, Kingunge Ngombale–Mwiru alisema wanatakiwa kumuenzi
Mandela kwa kufanya kwa vitendo mema aliyoyaacha,.
Kingunge alisema viongozi hawatakiwi kuhuzunika na kulia,
kwani aliyofanya Mandela yanatosha kusherehekea siyo kuhuzunika.
Alisema baada ya kifo cha Mwalimu Julius Nyerere kila mtu
alihuzunika na kuongea mambo mengi, lakini hakuna aliyetekeleza kwa vitendo
aliyofanya.
“Ukiangalia viongozi wa zamani na sasa wana tofauti kubwa.
Viongozi wetu wa sasa wakipata madaraka wanajifikiria wao kwanza badala ya
wananchi,” alisema.
Naye Waziri Mkuu Mstaafu, Fredrick Sumaye alisema tatizo
lililopo bara la Afrika, ni suala la Uongozi na Utawala Bora vitu ambavyo
vikifuatwa na kuzingatiwa vitasadia maendeleo.
“Ukishakuwa na uongozi na utawala bora, yale mambo ya
kienyeji hayatakuwapo hivyo kila mmoja anatakiwa kuiga aliyofanya Mandela na
Nyerere, tutaibadili Afrika,” alisema Sumaye.
Balozi wa Palestina nchini, Dk Nasri Abu Jaish alisema kifo cha
Mandela siyo pigo kwa wananchi wa Afrika Kusini na Afrika pekee, bali
dunia nzima kwa sababu ni mwalimu wa dunia. “Alikuwa mwalimu kwa
viongozi, hakuwabagua watu, aliwaunganisha na kusaidia nchi zingine,” alisema.