Rais Kikwete awasili leo na siri nzito

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete anatua nchini leo akiwa na lake moyoni kuhusu hatima ya baraza lake la mawaziri, baada ya kutengua uteuzi wa mawaziri wake wanne, wiki mbili zilizopita.
Rais Kikwete alikwenda Marekani, Desemba 18, mwaka huu kufanyiwa uchunguzi wa afya yake na akiwa huko, upepo wa kisiasa ulibadilika na kumlazimisha kuchukua hatua hiyo ambayo inampa wajibu wa kupanga upya safu yake ya uongozi.
Mawaziri ambao uongozi wao ulitenguliwa ni wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi, Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha, Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki na Uvuvi na Maendeleo ya Mifugo, Dk Mathayo David Mathayo.
Kung’oka kwao kunatokana na ripoti ya kamati ndogo ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kuhusu athari zilizotokana na utekelezaji wa Operesheni Tokomeza Ujangili, ambayo ilizua mjadala mkali kiasi cha wabunge kumshinikiza Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwamba naye aachie ngazi.
Hivyo kitendawili kingine kikubwa kinachomkabili Rais Kikwete ni iwapo ataamua kuendelea kufanya kazi na Pinda ambaye alishambuliwa na wabunge kwamba naye ang’oke kwa madai kwamba ameshindwa kusimamia utendaji serikalini.
Kwa mujibu wa Katiba ya nchi, Ibara ya 52(1) Waziri Mkuu ndiye mwenye madaraka juu ya kudhibiti usimamiaji na utekelezaji wa siku wa kazi na shughuli za Serikali.
Katiba inasema: “Katika utekelezaji wa madaraka yake, Waziri Mkuu atatekeleza au kusababisha utekelezaji wa jambo lolote au mambo yoyote ambayo Rais ataagiza kwamba yatekelezwe. Ibara ya 53 (1) inaeleza: “Bila kuathiri masharti ya Katiba hii, Waziri Mkuu atawajibika kwa Rais kuhusu utekelezaji wa madaraka yake.”
Hata hivyo, ni kama Rais Kikwete alishaamua kumwokoa Pinda pale alipompa maagizo kwamba alitangazie Bunge uamuzi wake wa kutengua uteuzi wa mawaziri wanne.
Ripoti hiyo iliyosomwa na Mwenyekiti wake, James Lembeli ilifichua kuwapo kwa vifo na mateso ya wananchi vilivyofanywa wakati wa operesheni hiyo iliyoendeshwa na askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), maofisa wa Usalama wa Taifa na Polisi.
Mbali ya pengo lililoachwa na mawaziri hao wanne, Rais Kikwete pia ndiye mwenye majawabu kuhusu hatima ya wale waliotajwa kuwa ni mawaziri mizigo kwa kushindwa katika utendaji wao, hasa ikizingatiwa kuwa shinikizo la kuwajibishwa kwao linatoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho yeye ni mwenyekiti wake.
Kitendawili cha Pinda
Zipo hoja kadhaa, iwapo Rais Kikwete atamwondoa Pinda kama ambavyo wabunge walisisitiza wakati wakichangia ripoti hiyo, huku wakirejea yaliyowahi kutokea serikalini lakini Waziri Mkuu huyo akakwepa kuwajibika.

Socials